Thursday, July 10, 2014

VAN GAAL ATOBOA SIRI YA KUSHINDWA KUINGIA FAINALI ASEMA WACHEZAJI WALIKACHA’ KUPIGA PENATI YA KWANZA
KOCHA wa Netherlands Louis van Gaal ametoboa kuwa alipata shida sana kumpata Mchezaji wa kupiga Penati ya Kwanza ilipofikia hatua ya Mikwaju ya Penati Tano Tano baada Timu yake na Argentina kutoka 0-0 katika Dakika 120 za Nusu Fainali ya Kombe la Dunia hapo Jana.
Kwenye Penati hizo, Argentina waliibuka kidedea kwa kushinda Penati 4-2 baada Holland kukosa Penati mbili zilizopigwa na Ron Vlaar na Wesley Sneijder na Kipa Sergio Romero kuokoa.
Beki Ron Vlaara ndie aliepiga Penati ya Kwanza.
Lakini Louis van Gaal, ambae Timu yake iliitoa kwenye Robo Fainali Costa Rica kwa Penati ambazo mbili kati yake ziliokolewa na Kipa wa Akiba Tim Krul alieingizwa Dakika za Mwishoni kwa ajili tu ya Penati, Jana alishindwa kutumia mbinu hiyo hiyo baada ya kuwa tayari washabadilisha Wachezaji Watatu.
Akiongea na Wanahabari mara baada ya Mechi, Van Gaal alisema: “Ile na Costa Rica ingetupa imani kwani tulipiga vizuri sana. Lakini tatizo lilikuwa nani apige ya kwanza na niliwaomba Wachezaji Wawili na mwishoe nikaangukia kwa Vlaar. Yeye ndie alikuwa Mchezaji bora hivyo angekuwa anajiamini mno. Lakini hii inaonyesha jinsi ilivyokuwa ngumu kupiga Penati kwenye Penati Tano Tano.”
Aliongeza: “Ni mbaya mno, kupoteza Mechi kwa Penati. Ukiondoa yote, tulikuwa sawa na wao, kama sio Timu bora. Inahuzunisha sana!”
Kwenye Mikwaju Mitano ya Penati, Lionel Messi alianza kuifungia Argentina na Ron Vlaar kukosa kwa Netherland baada Kipa kuokoa, kisha Arjen Robben akafunga na Ezequiel Garay kuipa Argentina 2-1.
Akaja Wesley Sneijder na kukosa kwa Kipa kuokoa huku Sergio Aguero akifunga na Argentina kuwa 3-1 mbele.
Dirk Kuyt akafunga kwa Netherlands na kuwa 3-2 lakini Maxi Rodriguez akapiga Penati ya 4 na Argentuna kushinda 4-2.
Shujaa wa Argentina ni Kipa wao Sergio Romero alieokoa Penati mbili za Ron Vlaar na Wesley Sneijder.
Argentina wamefika Fainali yao ya kwanza ya Kombe la Dunia tangu Mwaka 1990.
Hii ni mara ya pili Netherlands kushindwa Mikwaju ya Penati 5 katika Nusu Fainali ya Kombe la Dunia, na ya kwanza ilikuwa dhidi ya Brazil Mwaka 1998.
Argentina wataivaa Germany Jumamosi kwenye Fainali ya Kombe la Dunia Uwanjani Maracana Jijini Rio de Janeiro
Netherlands itacheza dhidi ya Brazil kusaka mshindi wa Tatu.

No comments: