Friday, February 6, 2015

AFCON 2015: GHANA WATINGA FAINALI KUWAVAA IVORY COAST JUMAPILI, MALABO WAGEUKA UWANJA WA VITA


WANA wa Nguli wa Soka Afrika, Abedi Ayew Pele, wameiongoza Nchi yao Ghana kuwateketeza Wenyeji Equatorial Guinea kwa kuichapa Bao 3-0 katika Mechi ya Nusu Fainali ya Mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika, AFCON 2015, iliyochezwa Nuevo Estadio de Malabo, Mjini Malabo.

Watoto hao wa Abedi Pele, Andre Ayew na Jordan Ayew, kila mmoja alipiga Bao moja na Wakaso kufunga jingine kwenye Mechi ambayo Ghana waliongoza 2-0 hadi Mapumziko lakini walishindwa kuingia Vyumba vya Kubadili Jezi wakati huo baada ya Mashabiki wa Wenyeji Equatorial Guinea kupandwa jazba na kuirushia Timu ya Ghana vitu na kulazimu Polisi kuingilia kati.
Huku Washabiki hao wakitangaziwa kuwa Mechi hiyo itavunjwa na ulinzi kuimarishwa Kipindi cha Pili kilichezwa na Ghana kupiga Bao lao la Tatu.
Bao za Ghana zilifungwa na Penati ya Jordan Ayew Dakika ya 42, Wakaso Dakika ya 45, na Andre Ayew Dakika ya 75.
Gemu hii ilisimama Dakika ya 84 baada ya Washabiki wa Ghana kukimbilia Uwanjani toka Jukwaani wakihofia usalama wao baada ya kushambuliwa na Mashabiki wa Equatorial Guinea. Baada ya Nusu Saa, kwa msaada wa Helikopta na Polisi, Mechi ilianza tena na kuchezwa Dakika zilizosalia huku Uwanja ukiwa mtupu baada ya Watazamaji wengi kuondoka.
Ghana, ambao washawahi kuwa Mabingwa wa Afrika mara 4 ingawa hawajatwaa Ubingwa huo tangu 1982, wanatinga Fainali kucheza na Ivory Coast ambayo haijawahi kuwa Bingwa ingawa safari hii imesheheni Mastaa kibao wanaocheza Ulaya.
Jumatano Usiku, kwenye Nusu Fainali ya kwanza, Ivory Coast iliichapa Congo DR Bao 3-1.
Fainali itachezwa Jumapili ndani ya Estadio de Bata, Mjini Bata.

No comments: