SIMBA YAANZA VEMA MAPINDUZI CUP YABAMIZA LEOPARD YA KENYA 1-0
![]() |
Wachezaji wa simba wakishangilia bao la kiemba |
BAO pekee la kiungo Amri Ramadhani Kiemba, jana usiku limeifanya klabu ya Simba SC iuanze vyema mwaka 2014 baada ya kuifunga AFC Leopard ya Kenya 1-0 katika mchezo wa ufunguzi wa Kombe la Mapinduzi, Kundi B, Uwanja wa Amaan, Zanzibar
Kiemba aliyetokea benchi dakika ya 47 kwenda kuchukua nafasi ya Awadh Juma Issa, alifunga bao hilo baada ya kuunasa mpira uliookolewa na beki wa Leopard, kufuatia Amisi Tambwe kujaribu kuunganisha krosi ya Ramdhani Yahya Singano ‘Messi’ dakika ya 77.
Sifa zimuendee Messi, ambaye alimlamba chenga ya maudhi beki ngongoti, Joseph Shikokoti kabla ya kutia krosi iliyozaa bao hilo.
Kwa ujumla Simba SC, ambayo jana ilioongozwa na kocha Msaidizi, Suleiman Abdallah Matola ilicheza vizuri zaidi kipindi cha pili na ingeweza kuondoka na ushindi mnene kidogo, kama washambuliaji wangekuwa makini zaidi.
Leopard nayo ilicheza vizuri zaidi kipindi cha kwanza, safu yake ya kiungo ikiongozwa na mkongwe Oscar Kadenge.
Kwa ushindi huo, Simba SC inashika nafasi ya pili katika Kundi B kwa pointi zake tatu, nyuma ya KCC ya Uganda yenye pointi tatu pia, ambayo iliilaza KMKM 3-2 katika mechi ya kwanza jioni ya jana.
Kocha wa timu ya taifa ya Italia, Cesare Prandile aliyekuwa mgeni rasmi, alikagua timu zote mbili kabla ya mechi hiyo na kwenda kuudunda mpira katikati ya Uwanja kuashiria ufunguzi wa michuano hiyo ya nane ya Kombe la Mapinduzi.
No comments:
Post a Comment