Friday, November 15, 2013

YALIYOJIRI KUELEKEA KOMBE LA DUNIA 2014 NCHINI BRAZIL

MACHO na masikio ya mashabiki wa soka barani Afrika yatakuwa yakitizama mechi tano muhimu zitakazochezwa Jumamosi, Jumapili na Jumanne ambazo ndio zitakazotoa wawakilishi watano watakaoliwakilisha bara hili katika michuano ya Kombe la Dunia 2014 nchini Brazil. Jumamosi tutashuhudia Ethiopia ikisafiri kuifuata Nigeria ili kujaribu kurekebisha makosa ya kufungwa mabao 2-1 katika mechi ya kwanza wakati huko jijini Casablanca, Morocco, Senegal itaikaribisha Ivory Coast ambao walishinda mechi ya kwanza iliyofanyika jijini Abidjan kwa mabao 3-1. Jumapili kutakuwa na mtanange mwingine wa kukata na shoka ambapo Tunisia wataifuata Cameroon jijini Younde baada ya kwenda sare ya bila ya kufungana katika mchezo wa kwanza uliofanyika Octoba. Ratiba hiyo itakamilika Jumanne ambapo Misri itakuwa na kibarua kigumu jijini Cairo cha kugeuza matokeo ya bao 6-1 walizochapwa na Ghana katika mchezo wa kwanza uliofanyika jijini Kumasi wakati Burkina Faso nao wakijaribu bahati yao mbele ya Algeria baada ya kuwafunga mabao 3-2 katika mechi ya kwanza.

GHANA WAOMBA KUONGEZEWA ULINZI ZAIDI.

MAAFISA wa Shirikisho la Soka la Ghana-GFA limewaomba wenyeji wao Misri ulinzi zaidi kama tahadhari wakati timu ya taifa ya nchi hiyo maarufu kama Black Stars itakapowasili jijini Cairo wiki ijayo. Maofisa wanne kutoka GFA waliwasili jana Misri kwa ajili ya kufanya mazungumzo na viongozi wan chi hiyo pamoja na kupata taarifa ya usalama pamoja na wawakilishi wa Shirikisho la Soka Duniani-FIFA. Mjumbe wa bodi wa Shirikisho la Soka la Misri, Ehab Laheita ambaye alihudhuria mkutano huo amesema maofisa hao wa Ghana waliomba ulinzi zaidi wakati timu yao itakapowasili jijini Cairo na muwakilishi wa Wizara ya Mambo ya Ndani aliwahakikishia hilo. Laheita aliendelea kudai kuwa viongozi hao walikagua Uwanja wa Air Defense utakaotumika kwa ajili ya mchezo huo na kuridhishwa nao na kuomba nafasi zaidi kwa ajili ya mashabiki wao. Maofisa hao waliongozwa na rais wa GFA Kwesi Nyantakyi, Abeid Ayew Pele, Alhaji Saeed Lartey na Ibrahim Sannie.

ETO'O ALALAMIKIA WACHEZAJI WENZAKE CAMEROON KUMBANIA.

MSHAMBULIAJI nyota wa klabu ya Chelsea, Samuel Eto’o anaamini kuwa baadhi ya wachezaji wenzake wa Cameroon wanajaribu kutomsaidia asishinde katika mechi yao ya mtoano ya Kombe la Dunia dhidi ya Tunisia. Kauli hiyo ya Eto,o imekuja wakati wakielekea katika mechi ya mkondo wa pili itakayofanyika jijini Younde baada ya ile ya kwanza iliyofanyika jijini Tunis Octoba timu hizo kwenda sare ya bila ya kufungana. Eto’o mwenye umri wa miaka 32 amedai kuwa wachezaji wenzake wamekuwa hawapeleki mipira ipasavyo anapokuwa mbele hivyo inampasa kurudi nyuma zaidi ili kwenda kutafuta mipira mwenyewe. Nyota huyo aliendelea kudai kuwa soka ni mchezo wa ushirikiano na mchezaji ana jukumu la kutoa pasi hata kama unayempa mpira huo ni adui yako hususani unapokuwa katika nafasi nzuri. Hata hivyo, kocha wa Cameroon Volker Finke amepinga vikali madai hayo ya Eto’o na kusisitiza hakuona tatizo kama hilo wakati wa mchezo wao uliopita waliotoka sare.

WACHEZAJI CROATIA KUMWAGIWA FEDHA KAMA WAKIFUZU KOMBE LA DUNIA.

SHIRIKISHO la Soka nchini Croatia limetoa kitita cha euro 500,000 kama motisha kwa wachezaji wa timu ya taifa ya nchi hiyo kama wakifanikiwa kufuzu michuano ya Kombe la Dunia itakayofanyika mwakani nchini Brazil. Croatia inakabiliwa na mechi mbili za mtoano dhidi ya Iceland ili kukata tiketi kwa ajili ya michuano hiyo. Mechi ya mkondo wa kwanza kati ya timu hizo inatarajiwa kuchezwa jijini Reykjavik baadae leo huku mechi ya mkondo wa pili ikitarajiwa kuchezwa jijini Zagreb Jumanne ijayo. Croatia ilifanikiwa kumaliza katika nafasi ya tatu kwenye michuano ya Kombe la Dunia mwaka 1998 iliyofanyika nchini Ufaransa lakini walishindwa kufuzu michuano iliyopita ambayo ilifanyika nchini Afrika Kusini.

No comments: