Tuesday, November 5, 2013

MWANAMKE AMDANGANYA MUMEWE KWAMBA AMETEKWA NYARA, AKUTWA AKIPONDA RAHA NA HAWARA

Bi Mary Njeri, wakati akiwa kituo cha polisi cha Karatina
POLISI wa Karatina, eneo la Nyeri nchini Kenya, wanamzuilia mwanamke aliyepatikana akiponda raha siku mbili baada ya kujifanya alitekwa nyara kwa lengo la kumlaghai mumewe Sh500,000.


Bi Mary Njeri, mwenye umri wa miaka 22, alipatikana katika nyumba moja ya wageni eneo la Thogoto, Kiambu, mnamo Jumapili mchana akiwa na mwanamume mwingine, baada ya kudai alitekwa nyara na watu wasiojulikana akielekea Karatina kutoka nyumbani kwake, eneo la Ngandu, Nyeri, Ijumaa iliyopita.

Polisi walisema Njeri alidai alitekwa nyara na wanawake wawili na mwanamume mmoja na wakamlazimisha kupanda gari walilokuwa nalo aina ya Probox.
Afisa mkuu wa polisi Karatina (OCPD), Bw Rashid Mohammed, alisema alipata habari za kutekwa nyara kwa mwanamke huyo Ijumaa jioni na akatuma maafisa wake mara moja kumtafuta katika maeneo waliyoshuku alizuiliwa.
“Kufuatia msururu wa visa vya utekaji nyara katika eneo la Kirinyaga, hatukutaka kuharibu dakika hata moja. Mimi binafsi niliongoza shughuli za kumwokoa na nikatuma maafisa wangu maeneo tuliyodhani angepatikana,” akasema Bw Mohamed.
Mume wa mwanamke huyo, Bw Peter Kabingu,  ambaye ni dereva  wa matatu (daldala), alisema mpwa wake alimpigia simu kumjulisha kuwa mkewe alitekwa nyara akielekea Karatina.
Alisema siku hiyo mkewe alikuwa amepanga kukutana na mpwa wake huyo ili wamsaidie dada yake kujiandaa kwa harusi.
“Tulikubaliana aje mjini (Karatina) adhuhuri kukutana na mpwa wangu ili wampeleke dada yangu kwa fundi kupima nguo ya harusi,” akaeleza Bw Kabingu.
Lakini mwendo wa Saa Kumi na Moja jioni mpwa wake alipokea ujumbe kutoka kwa Njeri akimwambia alitekwa nyara na kuwa yeye watekaji wake walikuwa wakielekea Kirinyaga.
“Nilijaribu kumpigia simu lakini ilikuwa imezimwa, nikajua mambo hayakuwa sawa,” akasema Bw Kabingu.
Anasema alitafuta msaada wa mwakilishi wa wadi yao ambaye alipiga ripoti katika kituo cha polisi cha Karatina na shughuli za kumtafuta mkewe zikaanza.
“Sikulala Ijumaa usiku nikiwaza kuhusu yaliyompata mke wangu ambaye tumeishi pamoja kwa miaka minne sasa. Nililazimika kumtunza mtoto wetu mdogo,” akaeleza Bw Kabingu.
Jumamosi asubuhi, alipokea simu kutoka kwa waliodaiwa kuwa watekaji nyara wakitaka fidia ya Sh500, 000 ili wasimuue mkewe.
Baada ya kujadiliana, watekaji nyara hao walimtaka awatumie Sh10,000 kwanza ili waweze kuwasiliana naye. Alisema alisaidiwa na marafiki kupata pesa hizo na akazituma kupitia nambari ya simu ya mkewe kisha akaanza kutafuta zilizobaki.
Wakati huo polisi walikuwa wakiendelea kumsaka mkewe na Jumapili asubuhi wakampata eneo la Thogoto Kaunti ya Kiambu akiwa na mpenzi wake, Peter Mugo.
Bw Kabingu alisema hakuamini alipoambiwa mkewe alipatikana akiponda raha na mwanamume mwingine kwa kutumia pesa alizokusanya kwa shida ili kumwokoa.
“Nimefanya niwezalo kumfurahisha. Nimekuwa nikimtimizia mahitaji yote na hatujawahi kukosana kwa miaka minne ya ndoa yetu. Sielewi ni kwa nini alinifanyia haya,” akasema Bw Kabingu huku akitokwa na machozi.
Alisema ataamua hatua ya kuchukua baada ya kushauriana na wazazi na wakwe wake.

No comments: