Sunday, March 17, 2013

WANACHAMA WA SIMBA WAUNG’OA UONGOZI WA RAGE
Mwenyekiti wa Mkutano wa dharura wa klabu ya Simba, Mohamed Wande
Wanachama wa simba

WANACHAMA wa klabu ya Simba, leo walifanya kikao cha dharura kwenye Hoteli ya Star Light Mnazi Mmoja jijini Dar na kuung’oa uongozi wa klabu hiyo uliopo madarakani chini ya Mwenyekiti wake, Ismail Aden Rage kufuatia mwenendo mbaya wa timu yao.

Wanachama hao wamekabidhi uongozi wa klabu hiyo kwa Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha, Rahma Kharus ‘Malkia wa Nyuki’ na kumrudisha kiongozi aliyejiuzulu hivi karibuni, Zacharia Hans Poppe. Wanachama hao wamesema wanatarajia kuitisha mkutano mkuu na kuwachagua viongozi wapya baada ya kumalizika kwa Ligi Kuu inayoendelea ili kuepusha kuivuruga timu.

Mkutano huo umefantika bila baraka ya uongozi wa sasa wa Simba.

Wanachama takribani 506 walihudhuria mkutano huo ambao umemalizika kwa wanachama hao kukubaliana kuuondoa madarakani uongozi wa Rage.

Alipoulizwa Mwenyekiti mteule wa Kamati ya Muda, Zacharia Hans Poppe, kwanza alisema hana taarifa za Mkutano huo wala yaliyofikiwa.

“Sina taarifa na wala siafiki, kwa sababu hakuna mtu aliyeshauriana na mimi kabla, na pia wamefanya mambo kinyume na Katiba,”alisema Kapteni huyo wa zamani wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ).

“Lazima wanachama wawe na subira, wasubiri Mwenyekiti arudi aitishe mwenyewe Mkutano, yeye mwenyewe (Mwenyekiti) alikwishasema ataitisha Mkutano, sasa kitu gani kinachowafanya wao wanakosa subira,”.

“Mbaya zaidi wamekwenda kufanya Mkutano wao na kufikia maamuzi yao, bila hata kunitafuta kuniuliza kwanza, sasa hii si ni dharau? Ina maana wao wanataka mimi nifanye wanavyotaka wao, mimi sitaki kuwa sehemu ya migogoro katika Simba,” alisema Hans Poppe.

No comments: